Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akitoka
kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha { AICC } Baada ya kuufunga
Mkutano wa Mafuta na Maonyesho wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Rais wa Zanzibar Dr. Ali
Mohammed Shein. Kulia ya Balozi ni Naibu Waziri wa Nishati na Madini wa
Tanzania Mh. George Simba Chawene, na kushoto yake ni Waziri wa Nishati wa
Uganda Mh. Irin Muloni na Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki
Mheshimiwa Jesca Eriyo.
Picha na Hassan Issa wa – OMPR –
ZNZ.
Na Othman Khamis Ame
Mataifa ya Jumuiya ya Kiuchumi ya
Afrika Mashariki { EAC } yametakiwa kuwa
makini katika mfumo na muundo mzima wa Sekta ya Mafuta na Gesi ambayo
inatarajiwa kuwa muhimili wa Uchumi mpya katika ukanda huu wa Bara la Afrika.
Wito huo umetolewa na Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein wakati akiufunga Mkutano wa Sita wa siku tatu
wa Mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki
kuhusu mafuta, Gesi na Maonyesho ya Taaluma ya Sekta hizo uliokuwa
ukifanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Arusha {AICC }.
Dr. Shein ambaye Hotuba yake
ilisomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali
Iddi alisema Ukanda wa Afrika Mashariki
hivi sasa unahitaji kuwa na sauti ya pamoja katika muundo huo
utakaowezesha Sekta hiyo kuyanufaisha
Mataifa hayo Wanachama katika Maendeleo
ya Kiuchumi.
Alisema Wawekezaji pamoja na Makampuni ya Kimataifa
yanayojihusisha na Sekta ya Mafuta na Gesi yanaweza kushajiika na mfumo
mzima wa ukanda huu kutegemea zaidi sera
na juhudi za Miundo mbinu itakayowekwa na Walaamu wa Mataifa hayo.
“ Ukanda wa Afrika Mashariki
umeonyesha dalili za mapema za kuwepo kwa rasilmali ya Mafuta na Gesi miaka
mingi iliyopita lakini kilichokosekana ndani ya muda huo ni utaalamu wa
Kuendesha Miradi inayotokana na Sekta hiyo”. Alifafanua Dr. Shein.
Alifahamisha kwamba idadi kubwa ya
Wawekezaji tayari wameshaonyesha nia ya
kutaka fursa ya kuwekeza katika Sekta ya Mafuta na Gesi ndani ya Ukanda wa
Afrika Mashariki baada ya Uganda
na Kenya kugundulika kuwa na
Mafuta na Gesi kwa Tanzania.
Aliwapongeza Viongozi na
Wataalamu wa Mataifa hayo ya Afrika Mashariki kwa juhudi zao zilizosaidia
kufanikisha Mikutano na vikao vilivyolenga kuimarisha Sekta hiyo mpya kwa
maendeleo ya Uchumi wa Mataifa yao.
Akimkaribisha Mgeni rasmi
kuufunga Mkutano huo wa Mafuta na Maonyesho Waziri wa Nishati wa Uganda Mh. Irin
Muloni alisema uendeshaji wa sekta ya Mafuta katika ukanda wa mataifa ya Afrika
Mashariki utaimarishwa ipasavyo kwa maslahi ya Mataifa hayo.Mh.
Mapema Katibu Mkuu wa Jumuiya ya
Afrika Mashariki { EAC } Mheshimiwa Jesca Erio amewahakikishia wawekezaji wote
watakaoamua kuwekeza kwenye sekta hiyo watajengewa mazingira bora ya
ushirikiano.
Mheshimiwa Jesca alisema
mazingira bora ya uwekezaji ndani ya sekta ya Mafuta katika Ukanda wa Afrika
Mashariki ni suala la msingi katika
kufanikisha na kuendeleza uchumi wa Mataifa hayo.
Akisoma maazimio ya Mkutano huo
Mhandishi Gosper alisema ipo haja
kwa Mataifa hayo kufanya juhudi za ziada
katika kuhakikisha Sekta hiyo inalindwa kwa vile inategemewa kubadilisha Uchumi
wa Mataifa Wanachama.
Mhandisi Gosper alifahamisha pia
kwamba suala la mazingira lazima litiliwe mkazo
kwa lengo la kulinda rasilmali zilizopo.
Mkutano wa saba wa Mafuta na
Maonyesho wa Mataifa ya Jumuiya ya Uchumi ya Afrika Mashariki unatarajiwa
kufanyika mwaka 2015.
No comments:
Post a Comment