Mwandishi Wetu
Kikosi cha timu ya Yanga kikifanya mazoezi nchini Uturuki |
Kocha huyo amekuwa mkali mara kadhaa kwani anataka wachezaji
wacheze soka la kasi ya aina yake, kwa kujiamini na wamekuwa wakimudu. Mara
kadhaa amekuwa akigombana na baadhi yao lakini humwelewa baadaye.
Katika mechi za vikosi viwili ambazo amekuwa akichezesha
wiki hii anasisitiza zaidi mfumo wa 4-3-3 jambo ambalo huenda likanogesha zaidi
mechi ya leo Jumamosi na kuwaduwaza Wajerumani hao.
Yanga ipo kamili na itawatumia wachezaji wake mahiri wa timu
za taifa kama beki Nadir Cannavaro, Kelvin Yondani, Didier Kavumbagu, Haruna
Niyonzima pamoja na mapacha Mbuyu Twite na Kabange Twite.
Huenda ikawa soka ya pasi na itakayonoga zaidi kwa mashabiki
ambapo kocha Brandts amesema kuwa ni kipimo kizuri na wanatarajia mechi
nyingine mbili wiki ijayo kujiweka fiti zaidi.
Ingawa hajasema mechi hizo ni dhidi ya timu gani, imebainika
kuwa ni za timu za miji ya hapa Antalya.
Hali ya hewa
Awali hali ya hewa ilikuwa baridi kali na mvua, lakini tangu
juzi Alhamisi na jana Ijumaa mambo yamebadilika ambapo mvua imekata na baridi
imepungua kwa kiasi kikubwa jambo ambalo limetoa nafasi kwa kocha na wachezaji
wa Yanga kujifunza mambo mengi.
Yanga imefikia kwenye hoteli ya kifahari ya Fame Residence
ambayo ipo karibu na Hoteli ya Mardan Palace ambayo ni ya nyota saba na ni ya
pili kwa kuwa ghali barani Ulaya.
Hoteli hiyo ya Mardan ndipo Bayern Munich ya Ujerumani
huweka kambi na muda wowote kuanzia sasa inadaiwa kwamba kuna timu moja kubwa
kutoka Ujerumani itatua hapo kwani tayari vyumba vimeshaandaliwa na wageni
hawaingii kwa wingi.
Katika hoteli ilipo Yanga kuna fukwe za kifahari ambazo kwa
saa 24 eneo kubwa hujaa wageni kutoka Ulaya.
Wageni hao hupendelea kuishi hapo kwa kuwa pamoja gharama
zake kuwa kubwa, huduma zake ni nzuri zinazokidhi pia viwango vya kimataifa.
Kiasi cha chini kulala kwenye hoteli hiyo kwa kichwa kimoja
ni Sh 140,000 kwa siku ambayo inahusisha chakula na kifungua kinywa.
Lakini kwa kuthibitisha ubora wa hoteli hiyo ya Yanga ni
kwamba mwezi huu wote imejaa na ukitaka chumba mpaka katikati ya mwezi ujao.
Yanga inajiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Bara
unaoanza Januari 26 na itatua Dar es Salaam Jumapili ijayo. Simba itaanza kambi
mjini Oman wiki ijayo.
No comments:
Post a Comment